Home » » MAKADA WA CCM KUMTOSA MGOMBEA ATAKAYEBEBWA

MAKADA WA CCM KUMTOSA MGOMBEA ATAKAYEBEBWA

BAADHI ya makada wakongwe wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wamesema watamkataa mgombea yeyote wa urais atakayeonekana kubebwa au kupata upendeleo kwa baadhi ya vigogo au kundi lolote kwa maslahi binafsi.

Kutokana na mchuano unaotarajiwa kuwepo kwenye kinyang’anyiro cha urais ndani ya CCM baadaye mwaka huu, baadhi ya makada wa chama hicho wamehofu kukiukwa baadhi ya taratibu na kanuni ili kupitisha mgombea kwa ujanja ujanja na kubebana.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na gazeti hili, makada hao Wamedai kutokana na mazingira yalivyo kuna kila dalili kuwa baadhi ya watu kutumia nafasi zao au kujuana kuhakikisha baadhi ya watu wanaibuka washindi kwenye mchuano huo.

"Tayari kuna tetesi kwamba familia yenye nguvu na ushawishi kisiasa hapa nchini, inadaiwa kusuka mpango kabambe kuhakikisha jina la mmoja wa vigogo wanaotajwa kuchuana kwenye nafasi hiyo linapenya na kuungwa mkono ndani ya vikao vya CCM hatimaye ‘mtu wao’ ateuliwe na CCM kugombea urais na hatimaye kurithi nafasi ya Rais wa sasa Jakaya Kikwete, atakapomaliza muda wake kikatiba Oktoba mwaka huu," alisema mmoja wa makada hao kwa sharti la jina lake kutochapishwa gazetini.

Alisema zipo taarifa kuwa familia hiyo sasa inafanya kila linalowezekana ikiwa ni pamoja na kusaidia kusaka pesa ndani na nje ya nchi ili kumsaidia kada huyo pindi kipenga cha mbio za urais ndani ya CCM kitakapopulizwa siku za karibuni.

Tayari vigogo wa CCM katika baadhi ya mikoa, wakiwemo wenyeviti, wamethibitisha kudokezwa suala hilo na kushawishiwa kuachana na wanachama wengine wenye nia ya kutaka nafasi hiyo, badala yake wasimame kumuunga mkono kigogo huyo, kinyume na hapo watakuwa wanapoteza muda wao kwani wengine hawana baraka zake.

Kigogo mmoja wa CCM kutoka Kanda ya Ziwa mapema wiki hii aliweka wazi suala hilo, huku akiwataka wagombea wengine kutopoteza.

“Mimi nawaheshimu sana watu wote wanaotajwa tajwa kugombea urais, lakini sina namna kwani tumeambiwa kuendelea kuwaunga mkono ni kupoteza muda. Familia ya (anataja) inamtaka (anataja). Tunamuunga mkono huyu kwani ndiye mwenye baraka hizo,” alikaririwa akisema kada huyo.

Taarifa za uhakika ambazo gazeti hili linazo, zinaeleza kuwa tayari mikakati kabambe inafanyika usiku na mchana kuhakikisha jina na sifa za kada huyo zinamwagwa kila kona nchini, huku mipango mingine ikisukwa kuhakikisha anapitishwa na vikao vya chama.

Akizungumza na gazeti hili kwa sharti la kuhifadhiwa jina, kigogo mwingine wa CCM Kanda ya Ziwa, alipinga vikali hatua hiyo na kuonya kuwa CCM itafanya makosa makubwa endapo itatoa mwanya kupata mgombea kwa shinikizo la kundi au mtu kwa maslahi binafsi, matokeo yake yatakigharimu chama hicho.

Alisema katika historia yake, CCM kimekuwa chama cha umma na viongozi wake wanapatikana kidemokrasia ambapo huungwa mkono na wanachama wote na kamwe hawatokani na sababu za urafiki au familia.

Alionya kuwa endapo suala hilo litabainika haitakuwa ajabu mgombea huyo wa kukataliwa vibaya na wana CCM jambo litakalokuwa aibu kwa pande zote mgombea huyo.

“Tuwaache wanachama waamue wanamtaka nani, kama ni kushindana uwepo ushindani sawa mwisho wa siku tupate mgombea anayekubalika na wengi, hapo tutashinda, kinyume na hapo itakuwa aibu, chama kitaparaganyika hata kuwapa mwanya wapinzani kuongoza dola.

Kama kuna watu au mtu anayejiona anaweza kutengeneza rais wake kwa sababua anazozijua yeye, anajidanganya, hiyo ni ndoto ya mchana kwa CCM ya leo, demokrasia ndani ya CCM ya leo ni kubwa, inatisha. CCM ya leo watu wasema ‘hapana’ tena mchana kweupe bila kumwonea mtu haya. Hatutakubali kamwe genge la watu au familia kuteka nyara nguvu ya chama kuteua mgombea wake,” alisema kada huyo.

Aliongeza kwamba CCM ina hazina kubwa ya viongozi hivyo hakuna sababu suala la uteuzi wa jina la mgombea urais kutekwa nyara na kundi au familia fulani, wanaotaka nafasi hiyo waachiwe wapambane kwa usawa vinginevyo atakayekuja kwa kubebwa atakataliwa.

“Sisi tunasubiri, haya mambo hayana siri, wakati ukifika yatakuwa wazi, kama kuna aliyebebwa na chama kimeporwa nguvu ya kutafuta mgombea wake.

Tutajipanga na kumkataa. Tutawakataa wagombea wote tutakaobaini wamebebwa. Tutawakataa ili kuwaonesha kuwa chama hakiburuzwi kupata mgombea wake," alisema.

Chanzo:Majira

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kigoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa