Home » » HOT NEWS: Urais waivuruga ACT ya kina Zitto.

HOT NEWS: Urais waivuruga ACT ya kina Zitto.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Zitto Kabwe.
Hali ya hewa ndani ya Chama cha ACT- Wazalendo ambacho kinaongozwa na Zitto Kabwe, imechafuka, baada ya Kamati Kuu kumpitisha na kumchukulia fomu ya urais, Prof. Kitila Mkumbo, huku mwenyewe akisita kulipokea jukumu hilo.
 
Kufuatia hatua hiyo, Prof. Kitila ameandika katika mtandao wa kijamii kuwa hajaandaliwa kisaikolojia kupeperusha bendera ya chama hicho katika nafasi ya urais na jukumu hilo wapewe viongozi wengine waandamizi.
 
Tofauti na ilivyozoeleka kwa wagombea kwenda na wafuasi wao Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) kuchukua fomu za kugombea urais, kwa upande wa ACT – Wazalendo, Katibu Mkuu, Samson Mwigamba, jana alikwenda Nec kumchukulia  fomu Prof. Kitila ambaye inadaiwa viongozi wakuu wa chama hicho wamekutana naye kwa mazungumzo ya kumshawishi akubali kupeperusha bendera ya chama hicho kuelekea Ikulu.
 
Mapema asubuhi jana Prof. Kitila alifika ofisi za chama hicho Kijitonyama na kuondoka na majira ya saa 5:00 asubuhi wafuasi zaidi ya 100 wakiwa na mabango yenye ujumbe mbalimbali walivamia ofisi hiyo na kumbana Mwigamba kuwaeleza kwanini chama hicho kinachelewa kuweka wazi mchakato wa mgombea wake wa urais. 
 
Habari zinasema kuwa licha ya Prof. Kitila kutokuwapo kwenye kikao cha Kamati Kuu (CC) kilichopitisha uamuzi wa kumtaka apeperushe bendera ya chama hicho katika nafasi ya urais, lakini ulipitishwa uamuzi wa kwamba abebe jukumu hilo zito.
 
Wakati Kamati Kuu kiamua hivyo, hadi jana alasiri hapakuwapo na makubaliano na Prof. Kitila, lakini viongozi wakuu wa chama walikuwa kwenye mazungumzo naye.
 
Akizungumza na Nipashe jana, Mwigamba alisema alichukua fomu hiyo saa 4:00 asubuhi, ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Kamati Kuu iliyokutana Agosti 15, mwaka huu.
 
Alisema pamoja na azimio hilo, Kamati Kuu ilipitisha majina ya wagombea ubunge nchi nzima, wagombea udiwani na kupokea ripoti ya wataalamu washauri juu ya ushiriki katika harakati za uchaguzi wa rais.
 
“Baada ya kupokea taarifa na mapendekezo yao tukajiridhisha kwa mustakabali wa taifa, chama kinahitaji kusimamisha mgombea urais, ndipo nilipoagizwa kwenda kuchukua kwa sababu muda unaenda zianze kujazwa ili Ijumaa ambayo ndiyo siku ya mwisho zirudishwe,” alisema Mwigamba.
 
Alisema Kamati Kuu imeamua hivyo kwa kuwa Prof. Kitila ni mwadilifu, mzalendo wa kweli, anaweka mbele maslahi ya Taifa na kwamba ana sifa zote za kuliongoza taifa na mgombea mwenza atakuwa ni Mwandishi wa habari mkongwe, Hawra Shamte. 
 
Hata hivyo, Hawra, alipoulizwa kuhusu maamuzi hayo ya Kamati Kuu, alisema hana taarifa zozote na kwamba hadi jana jioni hakuarifiwa chochote.
 
Alisema wakati mgombea huyo anakutana na viongozi wakuu wa chama hicho, fomu hiyo itaendelea kusambazwa mikoani ili kusaka wadhamini na kwamba walianza kufanya hivyo jana.
 
“Tofauti yetu na wengine hatutakuwa na ziara kwenye kusaka wadhamini, nimeenda na wanachama wengine watatu kuchukua fomu na sikuwa na msururu wa watu na hivyo hivyo kwenye kusaka wadhamini itakuwa kimya kimya,” alisema Mwigamba.
 
Alipoulizwa juu ya utayari wa Prof. Kitila kupeperusha bendera hiyo, alisema: “Hatuna wasiwasi, tunaamini atakubali uamuzi wa Kamati Kuu, anajua ni wajibu kubeba jukumu chama kinapomuhitaji.”
 
Aidha, Mwigamba alisema kama itashindikana kwa Prof. Kitila, ni lazima chama hicho kisimamishe mgombea mwingine katika nafasi hiyo.
 
KITILA: SINA MAANDALIZI
Katika kundi la mtandao wa kijamii la chama hicho la Whatsaap, lijulikanalo kama ACT Taasisi Imara, Prof. Kitila aliandika taarifa ya kuwashukuru wanachama na viongozi kwa imani yao kwake, lakini alisema hawezi kubeba jukumu hilo.
 
“Naomba niwashukuru nyote kwa imani kubwa mliyonayo juu yangu katika kukiwakilisha chama katika nafasi ya urais, naishukuru Kamati Kuu kwa imani yake kwangu hata kufikia hatua ya kupitisha azimio la kuniomba kugombea urais kwa chama chetu. Jana CC (Kamati Kuu) ilituma ujumbe maalum nyumbani kwangu kwa ajili ya kuzungumza na familia na jamaa zangu juu ya ombi hilo,” alisema katika andiko hilo na kuongeza:
 
“Nimekuwa nikitafakari tangu Alhamisi nilipoombwa rasmi kutafakari uwezekano wa mimi kugombea baada ya juhudi zetu za kutafuta mgombea kushindikana. Nimefanya mawasiliano mapana ndani ya familia, chama, chuoni ninapofanyia kazi, kanisani kwangu na kwa watu na taasisi mbalimbali ninazohusiana nazo.”
 
Alisema baada ya tafakari na mawasiliano mapana (consultations), ameona hana utayari na maandalizi ya maana ya kisaikolojia, kifamilia na kisiasa kumuwezesha kugombea nafasi ya urais katika uchaguzi mkuu ujao.
 
“Najua nimewaangusha sana katika uamuzi wangu huu, lakini naamini kwamba mtaheshimu uamuzi wangu na kwamba hamtaacha kuthamini mchango wangu katika chama kwa sababu ya kukataa kugombea urais,” alisema na kuongeza:
 
“Nasikitika kwa tuhuma ambazo baadhi ya wanachama wetu wanarusha katika mitandao ya kijamii na sehemu nyingine. Nathamini na kuheshimu haki ya wanachama kuonyesha hasira kwa jambo wasilolipenda…nawasihi wanachama wajizuie kuzusha mambo yatakayochochea chuki ndani ya chama na kukatishana tamaa.”
 
Aidha, alishauri wanachama wengine waandamizi waombwe wachukue jukumu hilo na kuwataja kuwa ni Mwenyekiti wa ACT – Wazalendo na Katibu Mkuu, Mwigamba na kwamba wakati hayo yakitafakariwa wasisahau malengo mapana ya chama waliyojiwekea katika uchaguzi huo.
 
Alisema mafanikio waliyofikia ni kuweka wagombea ubunge na udiwani kata na majimbo mengi nchini.
Mwigamba alipoulizwa juu ya taarifa hiyo, alijibu: “Sina simu ya whatsaap ila naenda kwenye kikao hadi leo (kesho) nitawapa taarifa.”
 
WAFUASI WAKUSANYIKA 
Baadhi ya mabango yaliyokuwa yamebebwa na wanachama na wafuasi wa ACT-Wazalendo yalikuwa na ujumbe wa ‘wamenunuliwa’ na mgombea wa Chadema, Edward Lowassa ili wasisimamishe mgombea urais.
 
Wafuasi hao walikaa kwa saa nne nje ya ofisi hizo wakiimba nyimbo mbalimbali.
 
 Mabango mengine yalisomeka: “Viongozi hatuwaelewi mmekaa muda mrefu bila kutuambia mgombea urais ni nani wakati muda unaisha, kama hamsimamishi mgombea ni bora mfunge ofisi, tusijihusishe tena na siasa, liko wapi azimio la Tabora?”
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kigoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa