Home » » Mradi wa vijana wamfurahisha Mratibu wa UN nchini

Mradi wa vijana wamfurahisha Mratibu wa UN nchini

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
IMG_6094
Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Kanali mstaafu Issa Machibya akiongozana na Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez mara tu baada ya kumpokea alipowasili ofisini kwake akiwa ameongozana na Ofisa wa Mambo ya Nje kutoka Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Maulidah Hassan, pamoja na Mwakilishi wa Shirika la Mpango wa idadi ya watu (UNFPA) nchini, Dkt. Natalia Kanem (hawapo pichani).
Na Mwandishi wetu, Kigoma
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez ameelezea kufurahishwa kwake na uwapo wa mradi wa kusaidia vijana wa kitanzania kujifunza ujasirimali na kujitegemea.
Akizungumza katika shughuli za uzalishaji mali za vijana wa Shirika lisilo la kiserikali la Nyakitonto Youth Development Tanzania la mjini Kigoma alisema kwamba shughuli wanazofanya vijana hao zinamsisimua sana.
 “Tunafurahi sana mimi na  wenzangu kutembelea mradi huu unaofadhiliwa na Shirika la Kazi Duniani (ILO) ambao unachochea ujasirimali miongoni mwa vijana. Sote tunajua kwamba vijana wengi wa Kitanzania wanaume kwa wanawake wameelimika lakini hawana ajira rasmi. Na suala la ujasiriamali ni kitu ambachio mtu anaweza kujifunza, na ujasiriamali unatoa fursa  kwa vijana kujiunga katika kundi la wafanyakazi kwa kujiajiri wenyewe.
“Tunajua kwamba kupitia shughuli zinazofadhiliwa na ILO katika ngazi ya jamii na kwa kufuata maelekezo ya serikalai za mtaa vijana wanaanzisha biashara mbalimbali binafsi au na jamii. Kiwanda cha kutengeneza sabuni ni mfano mzuri sana. Tunaona kwamba mradi huu unawaongezea kipato na hivyo kuweza kusaidia familia zao na kupeleka watoto shuleni na kuboresha lishe . Kwa ufupi mradi kama huu unasaidia kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazokabili kaya maskini Kigoma” alisema Rodriguez
ILO Kigoma inaendesha mafunzo ya ujasirimali kwa vijana kwa lengo la kuwawezesha kujiajiri wenyewe na  kuhudumia familia zao kwa kuziwezesha kupata huduma bora za elimu na afya kutokana na kipato chao.
IMG_6098
Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Kanali mstaafu Issa Machibya (kushoto) akibadilishana ‘Business card’ na Mwakilishi wa Shirika la Mpango wa idadi ya watu (UNFPA), Dkt. Natalia Kanem.
Alisema kwamba amefurahishwa na mradi huo ambao unawawezesha vijana kutambua fursa mbalimbali zilizopo na kuzitumia vyema kufanikisha maendeleo ya familia zao.
Aidha alisisitiza haja ya jumuiya ya kimataifa kuusaidia mkoa Kigoma katika nyanja mbalimbali za kiuchumi hasa katika eneo la ajira kwa vijana kutokana na ukarimu wa wakazi wa mkoa huo katika kuwapokea na kuwahudumia wakimbizi kutoka nchi za maziwa makuu kwa upendo.
Rodriguez alisema pamoja na ombi hilo Mratibu huyo wa shughuli za kimataifa ambaye ni Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo (UNDP) alisema wao kama UN wakifanyakazi pamoja wataendelea kutoa misaada kwa wakimbizi hasa uanzishaji wa miradi ya kiuchumi kwa vijana na wanawake.
Kwa upande wake Mwakilishi mkazi wa Shirika la Umoja wa mataifa la Idadi ya watu (UNPFA), Dkt. Natalia Kanem alisema kuwa kupatiwa mitaji na kuanzisha vikundi vya uzalishaji kwa vijana na wanawake kunasaidia kuongeza ajira lakini pia kusaidia kupunguza ongezeko kubwa la idadi ya watu bila mpangilio.
Katika risala yao kwa uongozi huo wa Umoja wa Mataifa vijana kutoka Nyakitonto Youth Development  Tanzania wamesema kuwa misaada iliyotolewa kwao imewasaidia kupata ujuzi na kuanzisha miradi ya uzalishaji mali ikiwa ni sehemu ya kujiajiri na kujiongezea kipato ili waweze kuendesha maisha yao bila utegemezi.
IMG_6105
Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Kanali mstaafu Issa Machibya akitoa taarifa ya mkoa wake kwa Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez aliyeambatana na ujumbe ofisini kwa Mkuu huyo wa mkoa.
Hata hivyo vijana hao katika risala yao iliyosomwa na Meneja miradi wa shirika hilo, Anjelina Gulanywa walisema kuwa pamoja na mafanikio hayo wanakabiliwa na changamoto utaalam mdogo, mitaji na vitendea kazi vya kisasa ili kufanya shughuli zao kuwa na mafanikio zaidi.
Naye Mkuu wa mkoa wa Kigoma, Kanali Mstaafu,  Issa Machibya alieleza kuridhishwa kwake na juhudi za Umoja wa Mataifa katika kusaidia miradi mbalimbali mikoani mwake ambayo inasadia wananchi kukabiliana na umaskini.
Mkoa wa Kigoma una mashirika mengi ya Umoja wa Mataifa yakifanya kazi mbalimbali za maendeleo na za kutoa huduma za kibinadamu kwa wakimbizi.
Mashirika hayo ya Umoja wa Mataifa yanayotekeleza miradi mbalimbali mkoani Kigoma ni pamoja na Shirika la Kuhudumia wakimbizi (UNHCR),Shirika la Afya Duniani ( WHO), Shirika la Mpango wa Idadi ya watu (UNFPA) ,Shirika la kazi la Kimataifa ( ILO), Shirika la Kuhudumia watoto( UNICEF), Shirika la Kuhudumia wahamiaji ( IOM), Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) na Shirika la maendeleo (UNDP).
IMG_6134
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez akielezea dhumuni la safari yake katika mkoa wa Kigoma kwa Mkuu wa mkoa huo, Kanali Mstaafu, Issa Machibya.
IMG_6123
Afisa Mawasiliano wa Shirika la Kimataifa la Kazi (ILO) nchini, Magnus Minja akitoa taarifa ya maendeleo ya mradi wa mafunzo ya ujasiriamali kwa vijana yenye lengo la kuwawezesha kujiajiri wenyewe na  kuhudumai familia zao kwa kuziwezesha kupata huduma bora za elimu na afya kutokana na kipato chao unaofadhiliwa na shirika hilo kwa Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Kanali Mstaafu, Issa Machibya.
IMG_6147
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez akiwasilisha Malengo 17 ya Maendeleo Endelevu (Sustainable Development Golas-SDGs) kwa Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Kanali mstaafu Issa Machibya. Kulia ni Mwakilishi wa Shirika la Mpango wa idadi ya watu (UNFPA) nchini, Dkt. Natalia Kanem.
IMG_6152
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez akikabidhi zawadi ya Khanga ya ‘miaka 60 ya UNFPA Tanzania’,  kwa Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Kanal Mstaafu, Issa Machibya, huku Mwakilishi wa Shirika la Mpango wa idadi ya watu (UNFPA) nchini, Dkt. Natalia Kanem akishuhudia tukio hilo.
IMG_6156
Malengo ya maendeleo endelevu sasa yamewafikia Kigoma. Pichani ni Mkuu wa mkoa wa Kigoma, Kanali Mstaafu, Issa Machibya na baadhi ya wakurugenzi katika ofisi ya mkuu huyo wa mkoa katika picha ya pamoja na ugeni kutoka Umoja wa Mataifa Dar es Salaam na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.
IMG_6161
IMG_6172
IMG_6164
Mkuu wa mkoa wa Kigoma, Kanali Mstaafu, Issa Machibya akiagana na Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez aliyemtembelea ofisini kwake kabla ya kuelekea kambi ya wakimbizi Nyarugusu.
KUELEKEA KWENYE UKAGUZI WA MRADI WA VIJANA UNAORATIBIWA NA ILO……..
IMG_6198
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez (kushoto) na Mwakilishi wa Shirika la Mpango wa idadi ya watu (UNFPA) nchini, Dkt. Natalia Kanem wakisikiliza taarifa ya waratibu wa mradi wa Vijana unaoratibiwa Shirika la  Nyakitonto Youth Development Tanzania la mjini Kigoma (NYDT)  na kufadhiliwa na ILO katika kuwawezeshaji vijana masuala ya ujasiriamali.
IMG_6216
Meneja miradi wa shirika hilo, Anjelina Gulanywa, Angelina Guranywa akitoa taarifa kwa Mkuu wa UN Tanzania (hayupo pichani) na ugeni wake alioambatana nao.
IMG_6230
Malengo ya maendeleo endelevu sasa yamewafikia Shirika lisilo la kiserikali la Nyakitonto Youth For Development Tanzania mkoani Kigoma.
IMG_6242
Baadhi ya vijana walionufaika na mradi wa ILO wa kuwezesha vijana kuwa wajasiriamali kwa kuwapatia mafunzo mbalimbali.
IMG_6250
Mratibu wa Shirika lisilo la kiserikali la Nyakitonto for Youth Development Tanzania, Joel Nyakitonto, akitoa maelezo kwa Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez jinsi utengenezaji wa sabuni kutokana mafuta ya mbegu za Mchikichi walipotembelea kiwanda cha Sabuni kilichopo tarafa ya Katubuka ambacho kinamilikiwa na kijana Diocres Dionizi (hayupo pichani) ambaye ni mmoja kati ya vijana 30 aliyenufaika na mafunzo ya Anzisha Biashara Yako (ABIYA) yaliyotolewa na taasisi hiyo kwa ufadhili wa Shirika la Kazi nchini (ILO).
IMG_6281
Wafanyakazi wa kiwanda hicho wakikusanya mbegu kwa ajili ya kukamuliwa kwenye mashine maalum.
IMG_6283
Ofisa wa Mambo ya Nje kutoka Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Maulidah Hassan akimtwisha ndoo ya mbegu za Mchikichi zinazokamuliwa na kupatikana mafuta yanayotengenezea sabuni za magadi mmoja wa wafanyakazi wa kiwanda hicho ambaye jina lake halikuweza kupatikana kiurahisi.
IMG_6291
Mwakilishi wa Shirika la Mpango wa idadi ya watu (UNFPA) nchini, Dkt. Natalia Kanem akimsaidia kujaza mbegu za Mchikichi mmoja wa wafanyakazi kiwandani hapo kwa ajili kuzichuja na kupata mafuta yanayotengenezea sabuni za magadi.
IMG_6307
Mwanamke aliyebeba mtoto wake mgongo huku akiwa amejitwishandoo yenye mbegu za Mchikichi kuelekea ndani ya kiwanda cha kusaga mbegu hizo zinazotoa mafuta yanayotumika kutengeneza sabuni za magadi kiwandani hapo.
IMG_6310
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez akivaa koti maalum kwa ajili ya kuingia kiwanda kujionea jinsi kijana huyo anayotengeneza sabuni za magadi zinazotokana mafuta ya mchikichi. Kushoto mmiliki wa kiwanda hicho kijana Diocres Dionizi aliyenufaika na mafunzo ya ABIYA yaliyofadhiliwa na ILO.
IMG_6327
Mfanyakazi wa kiwanda hicho kitengo cha ufungashaji bidhaa, Eric Mwesiga (27) akimwelekeza Ofisa wa Mambo ya Nje kutoka Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Maulidah Hassan (kushoto) namna wanavyopakia sabuni hizo kwenye mifuko maalum tayari kuingia sokoni.
IMG_6345
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez na Mwakilishi wa Shirika la Mpango wa idadi ya watu (UNFPA) nchini, Dkt. Natalia Kanem wakishuhudia maandalizi ya utengenezaji wa sabuni kiwandani hapo.
IMG_6353
Maandalizi yakianza kwa kumimina mafuta yaliyotokana na mbegu za mchikichi.
IMG_6395
Kijana Diocres Dionizi aliyenufaika na mafunzo ya ABIYA yaliyofadhiliwa na ILO akisaidiana na mfanyakazi wake  Erick Mwesiga kumwaga mchanganyiko huo kwenye chombo maalum huku Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez akishuhudia tukio hilo.
IMG_6398
Erick Mwesiga akichanganya rangi kwenye mchanganyiko ambao unakaa siku tatu mpaka kukauka na kupatikana sabuni za magadi.
IMG_6410
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez na Mwakilishi wa Shirika la Mpango wa idadi ya watu (UNFPA) nchini, Dkt. Natalia Kanem katika picha ya pamoja na Baba mzazi wa kijana Diocres Dionizi ambaye ni mjasiriamali wa sabuni.
IMG_6424
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez akiwasili kuzindua eneo la heka 3 la rasilimali na kuwaanda vijana (Youth incubation centre) ambalo limetolewa na  manispaa ya Kigoma/Ujiji kwa Taasisi isiyo ya kiserikali ya Nyakitonto Youth For Development Tanzania wanaojihusisha na kutoa mafunzo mbalimbali ya masuala ya ujasiriamali ikiwemo kuanzisha biashara.
IMG_6443
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez akikata kuzindua eneo la heka 3 la kituo cha mafunzo kwa vitendo kwa ajili ya kuwaanda vijana katika kilimo na ufugaji kuku (Youth incubation resource centre) ambalo limetolewa na manispaa ya Kigoma/Ujiji kwa Taasisi isiyo ya kiserikali ya Nyakitonto Youth For Development Tanzania kwa faida ya vijana Kigoma kujikwamua kiuchumi.
IMG_6445
IMG_6450
IMG_6466
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez akipata maelezo ya eneo la ndani litakalotumika kwa vitendo katika kilimo na ufugaji kwa vijana wa Kigoma ili waweze kujikwamua kiuchumi.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kigoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa