Home » » VIFO VYA WAJAWAZITO VYAPUNGUA.

VIFO VYA WAJAWAZITO VYAPUNGUA.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
KUFUNGULIWA vyumba vya upasuaji katika vituo vya afya zaidi ya 15 mkoani Kigoma na kupatiwa vifaa mbalimbali kwenye vituo hivyo kumeanza kutimiza lengo la mkoa huo kupunguza vifo vya wajawazito na watoto wakati wa kujifungua.
Kaimu Mganga Mkuu wa mkoa Kigoma, Dk Fadhili Kibaya, alisema hayo wakati wa kupokea seti 10 za Ombwe (Vacuum Extraction) zenye thamani ya Sh milioni 34.5 zilizotolewa na Shirika la World Lung Foundation zinazosaidia mjamzito mwenye matatizo kujifungua bila kufanyiwa upasuaji.
Dk Kibaya alisema kuwa, tangu kuanza kuboresha kwa vituo hivyo vya afya katika kipindi cha miaka minne iliyopita, wajawazito 18,281 wamejifungulia kwenye vituo hivyo na kati yao 1613 wamefanyiwa upasuaji.
Alisema, kuongezeka kwa wajawazito kujifungulia katika vituo rasmi vya utoaji huduma kumewezesha kupunguza vifo vyao kutoka 49 mwaka 2014 na kufikia vifo 39 mwaka jana.
Kwa upande wake, Katibu Tawala wa mkoa huu, John Ndunguru, alilishukuru shirika la World Lung Foundation, kwa programu yake ya kuboresha vituo vya utoaji huduma mkoani humu, ambayo imesaidia katika kutekeleza mipango ya serikali na malengo ya milenia katika kupunguza vifo vya wajawazito na watoto wakati wa kujifungua.
Hata hivyo, alisema kuwa ujio na ongezeko kubwa la wakimbizi vimefanya baadhi ya huduma ambazo zilizapangwa kwa Watanzania katika huduma za afya kuelekezwa kwa wakimbizi na ameomba serikali ya Burundi kudumisha amani nchini mwao ili kupunguza wimbi la wakimbizi nchini.
Awali, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la World Lung Foundation, Dk Nguke Mwakatundu alisema kuwa licha ya kufunguliwa kwa vyumba vya upasuaji katika vituo mbalimbali vya afya mkoani humo, kukabidhiwa kwa vifaa hivyo kutawezesha wajawazito wenye matatizo kujifungua kwa kutumia vifaa hivyo badala ya kufanyiwa upasuaji.
CHANZO ; HABARI LEO.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kigoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa