Home » » WATAKAOSHINDWA KUTEKELEZA CHF KUKIONA.

WATAKAOSHINDWA KUTEKELEZA CHF KUKIONA.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
SERIKALI wilayani Uvinza mkoani Kigoma imetangaza kuwachukulia hatua viongozi wa vijiji watakaoshindwa kutekeleza malengo yaliyowekwa katika kusimamia uhamasishaji wa jamii kujiunga na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF).
Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Mrisho Gambo alisema hayo akifunga kikao cha wadau kilichokuwa kikijadili mchakato wa upitishaji wa sheria ndogo ya Halmashauri ya kutambua na kusimamia utekelezaji wa huduma za mfuko wa afya ya jamii na bodi za afya katika wilaya hiyo.
Gambo alisema baada ya kikao hicho mkakati uliopo ni kuhakikisha wananchi wote wa wilaya hiyo wanajiunga na Mfuko wa Afya ya Jamii ambapo vijiji vimepewa malengo ya uandikishaji wa asilimia 80 kwa kaya huku watendaji wa vijiji wakiwa ndiyo wasimamizi wakuu wa utekelezaji wa mpango huo.
Alisema serikali haitasita kuwachukulia hatua za kinidhamu wajumbe wa bodi za usimamizi wa afya katika ngazi za kata na wilaya watakaoshindwa kusimamia utoaji huduma bora za afya katika maeneo yao kwa huduma hizo kugubikwa na malalamiko ya wananchi ikiwemo wizi wa dawa na kauli za unyanyasaji za watoa huduma.
Kwa upande wake, Ofisa Mwandamizi wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Ally Mwakababu kutoka mkoani Tanga alisema changamoto kubwa kwa sasa katika utoaji huduma kwenye sekta ya afya ni dawa, vitendea kazi na wataalamu.
Mwakababu alisema kujiunga kwa wingi kwa jamii katika NHIF na tiba kwa kadi kutawezesha halmashauri kutumia fedha inazopata katika kukabiliana na changamoto hizo na hivyo kuwezesha wananchi wanaotoa fedha zao kupata huduma bora wakati wote.
Akizungumza katika mkutano huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza, Omari Mkombole alisema kwa sasa hali ya uchangiaji wa wananchi katika CHF wilayani humo iko chini na sababu kubwa ni changamoto zilizopo kwenye utoaji huduma, hali ambayo baada ya mkutano huo mkakati umewekwa kuhakikisha asilimia 80 ya kaya 70,000 zenye jumla ya watu 400,000 zinajiunga na Mfuko huo.
 CHANZO : HABARI LEO.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kigoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa