Home » » Serikali yasaidia wakimbizi 55,320 Nduta

Serikali yasaidia wakimbizi 55,320 Nduta

Na Jacquiline Mrisho - Kigoma

Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania imewasaidia jumla ya wakimbizi 55,320 kutoka Burundi kwa kuwapa makazi na kuhakikisha ulinzi wa maisha yao katika Kambi ya Nduta iliyopo wilayani Kibondo, Mkoa wa Kigoma.

Takwimu hizo zimetolewa na Mkuu wa Kambi  hiyo, Peter Buluku wakati akizungumza na mwandishi wa habari hii juu ya hali halisi ya maisha ya wakimbizi wanaoishi katika kambi hiyo pamoja na misaada inayotolewa na Serikali pamoja na Mashirika yasiyo ya kiserikali.

Buluku amesema kuwa wakimbizi hao ni raia wa Burundi ambao wamekimbia nchini kwao kutokana na vurugu zilizojitokeza mwezi Aprili mwaka 2015 ambazo zilisababisha raia hao kukimbilia nchi za jirani ikiwemo Tanzania.

“Sisi kama Serikali tunasaidia wakimbizi kwa kuwapa ardhi kwa ajili ya makazi, kuhakikisha ulinzi na usalama kwa wakimbizi,kupokea, kusajili na kutunza kumbukumbu za wakimbizi  pamoja na kuunganisha familia za wakimbizi zilizopoteana  wakati wa machafuko nchini mwao”, alisema Buluku.

Alifafanua kuwa kazi ya kutoa huduma za kijamii zikiwemo za Afya, Chakula, ujenzi wa nyumba, masoko,vyuo vya ufundi na miundombinu, Maji, huduma za haki za watoto na wazee wasiojiweza, elimu pamoja na huduma za kutoa misaada ya kisheria zinafanywa na mashirika yasiyo ya kiserikali yaliyojitolea kuwasaidia wakimbizi hao.

Buluku aliongeza kuwa hadi sasa kuna jumla ya mashirika yasiyo ya kiserikali 17 yanayoshirikiana na Serikali kuhudumia Kambi hiyo ambapo huduma zote zinaongozwa na Shirika la Kuhudumia Wakimbizi Duniani (UNHCR) hivyo, kazi kubwa ya Serikali ni kusimamia na kuhakikisha mashirika yote yanatoa huduma zinazofaa kwa wakimbizi hao.
Mkuu huyo wa Kambi ametaja changamoto kubwa inayoikabili kambi hiyo kuwa ni upungufu wa rasilimali fedha kwa mashirika ambayo hali hiyo husababisha  baadhi ya shughuli za kuiwezesha kambi hiyo kutofanikiwa.
mwisho
      

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kigoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa