Home » » TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI - IDADI YA WAKIMBIZI KUTOKA BURUNDI YAONGEZEKA KATIKA KAMBI YA NYARUGUSU

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI - IDADI YA WAKIMBIZI KUTOKA BURUNDI YAONGEZEKA KATIKA KAMBI YA NYARUGUSU

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Mkimbizi kutoka nchini Burundi, Jacqueline Elulu (mwenye mtoto), akisubiri kupata huduma ya afya katika kituo cha Red Cross kinachotoa huduma za afya kwa wakimbizi walioko katika kambi ya Nyarugusu iliyoko wilayani Kasulu mkoani Kigoma. Shirika la Red Cross ni mojawapo ya wadau wanaoshirikiana na Serikali kutoa huduma za afya katika kambi ya Nyarugusu.
Mkimbizi kutoka Burundi akipata huduma ya maji katika moja ya vituo vya maji vilivyojengwa katika Kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu. Huduma za maji safi na salama ni mojawapo ya mambo yanayotiliwa mkazo ili kulinda afya za wakimbizi.
Wakimbizi kutoka nchini Burundi walioko katika kambi ya Nyarugusu wakiwa wamebeba shehena ya unga wa mahindi jana, muda mfupi baada ya kugawiwa chakula hicho Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia chakula (WFP), lililoweka kituo chake katika kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu wilayani Kasulu, mkoani Kigoma.

PICHA ZOTE NA KITENGO CHA MAWASILIANO YA SERIKALI, WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCH
https://encrypted-tbn0.gstatic.com/images?q=tbn:ANd9GcTviopQ4SacUFrZb2jUWuw0YugEodD2tGZ-Ffb8R_h2MBCYYHrl
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
IDADI YA WAKIMBIZI WA BURUNDI WANAOHIFADHIWA KATIKA KAMBI YA WAKIMBIZI YA NYARUGUSU YAONGEZEKA
Idadi ya wakimbizi kutoka Burundi wanaokimbia nchi yao na kuingia nchini Tanzania imefikia 91,661 kwa takwimu za Jumanne, tarehe 08 Septemba, 2015.  Wakimbizi hawa kwa sasa wamehifadhiwa katika Kambi ya Wakimbizi ya Nyarugusu iliyoko wilayani Kasulu mkoani Kigoma.

Tangu waanze kuingia mwezi Aprili mwaka huu, Wizara ya Mambo ya Ndani  ya nchi kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi (UNHCR) na wadau wengine imekuwa ikiwapokea na kuwapa hifadhi na huduma nyingine muhimu.  Huduma hizi ni pamoja na za ulinzi, chakula, maji, elimu na afya.
Kutokana na kuboreshwa kwa huduma za ulinzi, hali ya ulinzi na usalama katika kambi ya Nyarugusu na maeneo yanayoizunguka imeimarika ambapo upo usalama wa kutosha. Kazi hii inafanywa na Polisi kwa kushirikiana na vikundi vya ulinzi shirikishi vinavyojumuisha baadhi ya wakimbizi wanaoishi katika kambi hii.
Kuhusu huduma za afya, Serikali kwa kushirikiana na wadau wengine kama vile Shirika la Msalaba Mwekundu Tanzania (TRCS) imeimarisha huduma hizo kwa kuongeza idadi ya watendaji, vifaa na dawa. Kuimarishwa kwa huduma za afya kumesaidia kudhibiti magonjwa ya mlipuko na kukabiliana na magonjwa mengine yasiyo ya mlipuko.  Upatikanaji wa maji safi na salama na kutolewa kwa elimu ya usafi wa mazingira pia umesaidia kwa kiasi kikubwa kudhibiti magonjwa ya mlipuko.
Wakati huohuo huduma za elimu zimeimarishwa ambapo kiasi cha wanafunzi 3,889 wa elimu ya msingi na sekondari waliokuja na wazazi wao kutoka Burundi wameandikishwa na wanaendelea na masomo.
Kabla ya kufikia idadi hii ya sasa, wengi wa wakimbizi hawa walianza kuingia kwa maelfu kupitia kijiji c,,ha Kagunga kilichopo mpakani na nchi ya Burundi ambapo idadi ilianza kupungua kidogo kidogo lakini kwa siku za hizi karibuni wakimbizi hawa wameendelea kuingilia wakiwa katika vikundi vidogovidogo kupitia katika vijiji vingine vya mpakani na nchi ya Burundi.
Vijiji hivyo ni pamoja na Kilelema, Kitanga, Helushingo, Migongo,na Kigadie vilivyopo wilayani Kasulu na Mabamba na Katanga wilayani Kibondo na Kituo kidogo cha Uhamiaji cha Manyovu kilichopo mpakani na nchi ya Burundi.  Aidha wakimbizi wengine wamekuwa wakipitia vijiji vya Bugarama, Kabanga na Kasange vilivyopo wilayani Ngara mkoani Kagera.
Wakimbizi hawa ambao wamekuwa wakipokelewa katika maeneo haya wamekuwa wakisajiliwa na hatimaye kusafirishwa hadi kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu ambapo kambi hiyo imekuwa ikipokea wastani wa wakimbizi mia mbili (200) kwa siku.
Hata hivyo kutokana na msongamano katika kambi hiyo ya Nyarugusu ambayo awali ilianzishwa mahsusi kwa ajili ya kuhifadhi wakimbizi kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia Wakimbizi (UNHCR) na wadau wengine ina mpango wa kuwahamisha wakimbizi hawa kutoka Burundi kwenda kwenye maeneo mengine.
Maeneo hayo ambayo yameshaanza kufanyiwa maandalizi ni Mtendeli na Karago wilayani Kakonko na Nduta wilayani Kibondo. Zoezi la kuwahamisha wakimbizi hawa kutoka Burundi linatarajiwa kuanza mwishoni mwa mwezi huu.
Kuhamishwa kwa wakimbizi hawa kutoka Burundi kutaondoa msongamano uliopo katika Kambi ya Nyarugusu ambayo itaendelea kuhifadhi wakimbizi kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).

IMETOLEWA NA:
Isaac J. Nantanga
(0754 484286)
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
Nyarugusu - KIGOMA

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kigoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa