Home » » Machali ahoji wizi wa dawa hospitalini

Machali ahoji wizi wa dawa hospitalini



MBUNGE wa Kasulu Mjini, Moses Machali (NCCR-Mageuzi), amehoji kama serikali imedhamiria kukomesha tabia ya uzembe na wizi unaosababisha ukosefu wa dawa katika hospitali nyingi nchini.
Pia mbunge huyo alihoji kama serikali ipo tayari kuipatia madaktari wa kutosha Hospitali ya Wilaya ya Kasulu ambayo ina upungufu mkubwa wa madaktari na madaktari waliopo wamekuwa wakikataa wenzao wasipelekwe kwa kuhofia kuchukua nafasi zao.
“Changamoto nyingi za ukosefu wa dawa zinatokana na wizi na uzembe wa watendaji. Serikali iko tayari kuhakikisha jambo hilo linakoma mara moja?” alihoji Machali.
Katika swali la msingi, mbunge huyo alitaka kujua mpango wa serikali wa kuongeza watumishi kwenye Hospitali ya Wilaya ya Kasulu ambayo wastani wa watumishi wa afya ni 600, lakini kwa mujibu wa taarifa ya Mganga Mkuu wa Wilaya (DMO), watumishi waliopo ni 186.
Akijibu maswali hayo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Hawa Ghasia, alisema serikali inapeleka watumishi katika maeneo yote kadiri wanavyopatikana kulingana na mahitaji.
Alisema serikali inatambua upungufu wa watumishi wa sekta ya afya nchini na kuongeza kuwa imeweka mkakati maalumu wa kuajiri wahitimu wote wanaomaliza vyuo vya afya.
Alisema Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu kwa sasa ina watumishi 359 wa kada mbalimbali za afya wakiwamo madaktari na wauuguzi wanaotoa huduma za afya kwenye Wilaya ya Kasulu.
Alisema Hospitali ya Wilaya ina watumishi 206, vituo vya afya vina watumishi 52 na zahanati zina watumishi 101.
“Kwa kuzingatia umuhimu wa watumishi wa kada za afya katika mwaka wa fedha 2012/2013 serikali ilitoa kibali cha kuajiri watumishi 41 wa sekta ya afya ambapo hadi Oktoba mwaka huu watumishi 28 wa kada za afya wamesharipoti katika Halmashauri ya Wilaya  ya Kasulu,” alisema Ghasia.
CHANZO;TANZANIA DAIMA

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kigoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa