Home » » JIPANGE MWAKA 2015 UWE WA MAFANIKIO KATIKA ELIMU

JIPANGE MWAKA 2015 UWE WA MAFANIKIO KATIKA ELIMU

 Saa zinahesabika kuukaribisha mwaka mpya wa 2015. Ninaungana na vijana wenzangu katika kudumisha amani katika kipindi chote cha sikukuu ili tuweze kusherehekea kwa amani.
Mengi tumeyajadili kwa kipindi chote cha mwaka huu kwa kushirikiana na Mwalimu Athuman Hayeshi pamoja na mhariri wa makala za elimu, Abeid Poyo kwa lengo la kuwapa maarifa wanafunzi kwa namna hii gazetini.
Ninaamini maarifa tuliyokuwa tunayatoa hapa yamewanufaisha wanafunzi na wapenzi wasomaji wa gazeti hili. Pongezi nyingi tunazirudisha kwenu mliochangia mada mbalimbalia ambazo zilijadiliwa hapa.
Wanafunzi walio katika madarasa ya mitihani wanapaswa kujiwekea malengo yao kuanzia sasa. Watakaoingia kidato cha pili watambue kwamba masomo yatakapoanza muda wa kusoma ni sasa. Tabia ya kusoma karibu na mtihani inapaswa kuachwa kwani haiwezi kumsaidia mwanafunzi kama wengi wao wanavyofikiri.
Wanafunzi wanaoingia kidato cha nne wafikirie zaidi kwamba wana muda mfupi kutokana na mwaka 2015 kuwa na hekaheka nyingi ukianza na kura ya maoni, kampeni za uchaguzi, uandikishaji wa daftari la kupika kura japokuwa haviwezi kuwaathiri katika masomo yao lakini jambo la kuzingata kwamba wana muda mfupi.
Kwa mwanafunzi ambaye ana kiu ya kusonga mbele iwapo amepata wastani asioridhishwa nao, ni kukaa chini na kutafakari kwa kina tatizo lipo wapi. Unaweza kujiuliza iwapo tatizo ni wewe mwenyewe, je, uweke mikakati gani ili uweze kupiga hatua katika mitihani ya robo muhula, nusu muhula na ile ya majaribio.
Ratiba ya kujisomea ni jambo la msingi kwa mwanafunzi yeyote. Kila mwanafunzi anafahamu uwezo wake.
Jambo lingine la msingi la kukumbushana kwa wanafunzi wote, muda ambao mwalimu hayupo darasani siyo muda wa kupiga soga na kuhadithiana masuala ya mitandaoni au habari zisizo na manufaa kwako, tumia muda wako vizuri kwa kujisomea.
Kwa mwanafunzi yeyote kusoma isiwe sababu ya kutoshirikiana na wazazi katika kazi nyingine za nyumbani. Mtoto mwenye tabia njema anapanga vyema ratiba yake ya shule pia anashirikiana na familia yake katika kazi zile anazomudu.
Suala la matumizi ya simu au mitandao inaweza ikawa kikwazo kwa mwanafunzi ambaye hatakuwa msikivu kwa wazazi au walimu kuhusu kuacha matumizi yasiyofaa. Jiwekee utaratibu wako mwenyewe hasa kujidhibiti katika matumizi ya simu na mitandao ya kijamii isiyo na manufaa kwako.
Ifaye simu yako na intaneti kama sehemu ya kukuongezea maarifa kitaaluma siyo vinginevyo.
Epuka makundi yasiyofaa. Mzazi anaweza kukushauri kuhusu marafiki wa kuwa nao kwa manufaa yako ya baadaye. Siyo kila rafiki anaweza kukufaa kwani wengine wana mawazo ambayo baadaye unaweza kujikuta unakwama katika masomo yako kutokana na kuchagua marafiki wenye ushauri mbaya.
Ni vyema kila mwanafunzi atambue kwamba hatima ya mafanikio yake ipo mikononi mwake mwenyewe. Malengo na mipango yako mizuri katika mwaka ujao ndiyo mafanikio yako katika elimu.
Jizatiti, pale ambapo ulilegalega mwaka 2014 rekebisha makosa ya utoro, uvivu wa kuamka mapema, kutofanya mazoezi ya darasani kwa wakati. Pia futa kauli kwamba ‘nitasoma kesho’ kwani Waswahili wanasema linalowezekana leo lisingoje kesho
Chanzo:Mwananchi
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kigoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa