Home » » POLISI KIGOMA YAANZISHA KUMBUKUMBU ZA BODABODA

POLISI KIGOMA YAANZISHA KUMBUKUMBU ZA BODABODA



Na Frank Geofray-Jeshi la Polisi, Kigoma
Jeshi la Polisi Mkoani Kigoma limeanzisha mfumo wa kuweka kumbukumbu za waendesha bodaboda wote katika wilaya ya Kigoma ili iwe rahisi kuwapatia mafunzo na kuwasaidia pindi wanapopata matatizo pamoja na kukabiliana na ajali za barabarani.
Hayo yalisemwa jana na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kigoma Kamishna Msaidizi wa Polisi Frasser Kashai wakati wa hafla fupi ya kuwakabidhi makoti maalumu waendesha bodaboda 350 kutoka vituo 15 vya Wilaya ya Kigoma yatakayowawezesha kutambulika maeneo wanapopaki pikipiki zao na kuwasaidia pindi wawapo barabarani.
Alisema Mfumo huo maalumu wa kuwatambua waendesha bodaboda utawasaidia sana abiria na waendesha bodaboda hasa pale wanapopata matatizo pindi wawapo barabarani kwakuwa itakuwa rahisi kuwatambua.
Kamanda Kashai alisema kuwepo kwa Mfumo huo kutawasaidia pia abiria kwa kuwa kutawapa fursa kujua  wanapanda pikipiki inayopaki eneo gani hasa kwakuangalia nyuma ya  makoti maalum waliyowapatia.
Aidha katika hatua nyingine Kamanda Kashai ametoa wito kwa waendesha bodaboda wengine katika Mkoa wa Kigoma kuiga mfano wa Wilaya ya Kibondo ambayo imefanikiwa sana katika suala la mpanda pikipiki kuvaa kofia ngumu yeye pamoja na abiria wake.
“Natoa wito kwa wilaya nyingine za Mkoa wa Kigoma za Kasulu,Uvinza, Kakonko na Buhibwe nao waige mfano wa waendesha bodaboda wa Kibondo kwakuwa wao wapo mbali sana katika suala hili la kujilinda na kutambuana hali ambayo inawafanya kuaminiwa na abiria wao” Alisema Kamanda Kashai
Kwa upande wao waendesha bodaboda katika wilaya ya Kigoma wamesema wataendelea kuwashauri wenzao kujiunga katika vikundi ili waweze kutambulika na kupata manufaa ambayo yatawaweka katika hali ya usalama wao, abiria pamoja na pikipiki zao.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kigoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa