*Mahasimu wamvaa ndani na nje ya Chadema
*Atamba kuushangaza mtandao unaomwinda
*Katibu wa Bunge amtetea, ampinga Werema
JINA la Zitto Kabwe, mwanasiasa kijana ambaye mvumo wa sifa zake
umechukua mwelekeo tofauti katika siku za hivi karibuni, limeendelea
kutawala mwenendo wa siasa za kitaifa kwa wiki ya tatu mfululizo sasa.
Zitto,
mmoja wa wabunge vijana ambao wametokea kuwa na ushawishi mkubwa ndani
na nje ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) ambacho yeye ni
mwanachama wake amejikuta akikabiliwa na tishio la kuanguka au
kuangushwa kisiasa na makundi ya mahasimu wake ambayo yanaonekana
kujipanga kummaliza.
Wakati
hatma ya kisiasa ya mwanasiasa huyo ikiendelea kubakia kuwa kitendawili
tangu Kamati Kuu ya Chadema itangaze kumvua nyadhifa zake zote za
kisiasa siku 22 zilizopita, wiki hii Zitto alijikuta akikabiliana na
mashambulizi makali ya maneno na misuto ndani ya Bunge.
Kinara
wa mashambulizi ya safari hii dhidi ya Zitto alikuwa ni Mwanasheria
Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema ambaye mbali ya kumwita Zitto
mwongo alikwenda mbele zaidi na kutoa tishio la kuchukuliwa kwa hatua za
kisheria dhidi ya mbunge huyo.
Werema
alitoa kauli hizo za mashambulizi na vitisho kutokana na kauli
iliyotolewa na Zitto bungeni aliyeituhumu serikali kwa kutokuonyesha
kuwa na nia ya dhati katika kuhakikisha kuwa, fedha zilizofichwa nje ya
nchi na baadhi ya Watanzania zinarejeshwa.
Akijibu
kauli hiyo ya Zitto, Werema alimshambulia mwanasiasa huyo kwa kushindwa
kutoa ushirikiano wa kutosha kwa kamati iliyoundwa na serikali
kulifuatilia suala hilo.
Werema
ambaye misimamo yake ndani ya Bunge katika siku za karibuni imekuwa
ikiibua utata mkubwa alifikia hatua ya kumtuhumu Zitto kwa kukiri akiwa
chini ya kiapo kwamba, alikuwa hana majina ya watu walioficha mabilioni
ya fedha katika akaunti nchini Uswisi, kinyume na kauli ambazo amekuwa
akizitoa ndani ya Bunge.
Kwa
sababu hiyo basi, Jaji Werema aliliambia Bunge kuwa serikali ilikuwa
ikitafakari namna ya kuchukua hatua za kisheria dhidi ya Zitto kwa madai
kwamba mbunge huyo alilidanganya Bunge kwa kudai kuwa ana majina ya
watu wanaodaiwa kuficha fedha na mali haramu nje ya nchi wakati si
kweli.
“Katika
hili, nawashukuru wabunge 87 waliofika mbele ya kamati, nawashukuru
wananchi wengine waliofika kwani sasa tumefika pazuri ila serikali
inaomba iongezewe miezi sita ili ikamilishe jambo hili lakini hili suala
la Zitto tutashughulika nalo kisheria kwa sababu huwezi kulidanganya
Bunge halafu ukaachwa,” alikaririwa Jaji Werema akiliambia Bunge.
Kama
ilivyokuwa kwa Werema, Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema (Chadema)
alionekana kutumia fursa hiyo kumshambulia Zitto ndani ya Bunge akimtaka
mwanachama huyo mwenzake wa Chadema na Mwanasheria Mkuu wa Serikali
“kutochezea akili za Watanzania katika sakata hilo.”
Lema
ambaye siku chache tu kabla ya Kamati Kuu ya Chadema haijachukua uamuzi
wa kumvua Zitto nafasi zote za uongozi aliingia katika mzozo na
mwanasiasa huyo, alikwenda mbele zaidi na kutaka apewe yeye majina ya
watu hao walioficha fedha Uswisi ili aweze kuwataja.
Akizungumza
na Rai Jumapili jana, Zitto alieleza kushangazwa na kauli hizo akisema
zilikuwa zimebeba kile ambacho alipata kukieleza kuhusu kuundwa kwa
mtandao wa kuhakikisha unammaliza na kuzima kabisa hoja yake ya
ukwapuaji wa mabilioni ya fedha za umma.
“Nilipata
kulisema hili la kuundwa kwa mtandao wa kunimaliza. Sasa hivi kila mtu
ambaye amepata kuumizwa na Zitto anajitokeza kunishambulia. Katika kundi
hilo iko mitandao ya urais wa mwaka 2015 ambayo inaundwa na watu
walioficha fedha Uswisi na kwingineko nje ya nchi,” alisema Zitto.
Mbali
ya hilo, Zitto alieleza kusikitishwa na kile alichokieleza kuwa ni
uongo wa wazi wa Jaji Werema bungeni akisema alikuwa hajawahi hata mara
moja kuhojiwa na kamati iliyoundwa na serikali kufuatilia suala hilo
akiwa chini ya kiapo.
“Siku
zote nimekuwa nikikataa kuhojiwa na kamati nje ya maeneo ya Bunge ili
kuwa na kinga kwa kile nitakachosema. Kwanza sijapata kuhojiwa nikiwa
chini ya kiapo. Ni kwa sababu hiyo wiki ijayo nitafanya kila niwezalo
ili kueleza ukweli kuhusu jambo hili,” alieleza Zitto.
Hakuishia
hapo, Zitto alieleza kulipuuza tishio la Jaji Werema kuhusu yeye
kuchukuliwa hatua za kisheria kwa kusema uongo, akisema hoja ya
mabilioni ya Uswisi si yake ingawa ni yeye aliianzisha kwani tayari
ilishachukuliwa na kuwa Azimio la Bunge.
“Mtafuteni
Katibu wa Bunge alieleze hili la miye kushitakiwa. Ni Umbumbumbu
kushangilia hoja ya Werema. Nawashangaa wanaoshangilia uongo ule. Hoja
ya mabilioni ya Uswisi si yangu tena ni ya Bunge.
“Huu
ni wakati ambao mwanasiasa anakomazwa, sitetereki hata kidogo.
Nitawashangaza wanaoshangilia hoja za uongo za Jaji Werema,” alisema
Zitto kwa kujiamini.
Rai
Jumapili lilipomtafuta Katibu wa Bunge, Thomas Kashililah na kumuuliza
kuhusu sakata hilo na tamko la Werema dhidi ya Zitto alieleza
kushangazwa na upotoshwaji unaofanywa.
“Hapa
hakuna hoja ya Zitto. Nadhani lipo tatizo la uelewa katika masuala ya
Bunge. Suala la mabilioni ya Uswisi ni Azimio Namba 9 la Bunge,” alisema
Kashililah.
Gazeti
hili lilipotaka aeleze maoni yake basi kuhusu kauli ya Werema kwanza
alikataa kusema ilikuwa ni ya ukweli au uongo bali aliifananisha hoja
hiyo na ile hoja ya migogoro ya ardhi iliyotolewa na Mbunge wa Kawe,
Halima Mdee (Chadema) ambayo nayo ilichukuliwa na kuwa ya Bunge baada ya
kuridhiwa na kupitishwa.
Ingawa
si rahisi kueleza moja kwa moja kuhusu usahihi au upotoshaji wa hoja ya
Werema, ni wazi hoja yake alikuwa akiielekeza katika Kanuni za Kudumu
za Bunge, Sehemu ya tano, Kifungu cha 64 (a) ambacho kinakataza mbunge
kutoa taarifa ambazo hazina ukweli ndani ya Bunge.
Kwa
mujibu wa kitabu cha kanuni za Kudumu za Bunge, sehemu ya sita, kanuni
ya 73 (3) inatoa mamlaka kwa spika kumsimamisha mbunge kuhudhuria vikao
visivyozidi vitano vya Bunge.
Katika
kitabu hicho chicho cha kanuni ya 74 (5) inaipa Bunge mamlaka ya
kuchukua hatua nyingine za kinidhamu, ikiwa ni pamoja na kumsimamisha
kazi mbunge yeyote aliyetenda kosa chini ya kanuni hii.
Nje
ya mwenendo na kanuni za Bunge kauli za Lema na Werema dhidi ya Zitto,
zinatoa taswira kwamba mbunge huyo anapita katika nyakati za hatari
kisiasa.
Ni
wazi kwamba, Werema kwa kujua au kutojua, kwa kukusudia au kwa bahati
mbaya alitoa kauli ile huku akijua ilikuwa ikichochea moto dhidi ya
Zitto ambaye kwa sasa yuko katika uhusiano mbaya na viongozi wenzake
kadhaa wakuu ndani ya Chadema.
Sakata
la vigogo wanaodaiwa kuficha mali na fedha haramu nje ya nchi limezua
mjadala mkubwa nchini huku serikali ikichukua muda mrefu kuwasilisha
ripoti katika mikutano takribani minne ya Bunge kama ilivyoahidi na sasa
imeomba miezi sita zaidi kufanyia kazi suala hilo.
Tangu
Zitto awasilishe hoja hiyo Novemba mwaka jana, na serikali kuchukua
hatua ya kuunda kamati ya kuchunguza, suala hilo limeonekana kuwagusa
watu mbalimbali ambapo miongoni mwa watu wanaotajwa kuhojiwa mpaka sasa
ni pamoja na wafanyabiashara wakubwa nchini akiwamo Mwenyekiti wa Taifa
wa Chadema, Freeman Mbowe na Mbunge wa zamani ya Igunga, Rostam Azizi
Na pamoja Blog
0 comments:
Post a Comment