Serikali wilayani Kakonko mkoani Kigoma, imelipiga marufuku kanisa moja la dini ya Kikristo linaloitwa Sabato Matengenezo, ambalo limeanzishwa na watu sita ambao kwa sasa wanashikiliwa polisi.
Waumini hao wanadaiwa kuwanyima haki za msingi 
watoto wao, ikiwamo kuwakataza kwenda shule, kupata matibabu katika 
hospitali na zahanati kwa kile wanachodai kuwa imani ya dini yao 
hairuhusu.
Habari kutoka kijijini hapo, zinasema kutokana na 
tukio hilo, watoto wawili wamefariki dunia baada ya wazazi wao kuacha 
kuwapeleka hospitali kwa kile walichodai kuwa ni kimyume na imani ya 
dini yao.
Hata hivyo, Kaimu Kamanda wa Polisi Kigoma, Dismas
 Kisufi alipoulizwa kuhusiana na tukio hilo pamoja na vifo hivyo alisema
 hajapata taarifa ya tukio hilo.
Mkuu wa Wilaya ya Kakonko, Peter Toyima naye 
alipoulizwa kuhusiana na tukio hilo, alikiri kuwa na taarifa kuhusu 
kanisa hilo na kusema kanisa hilo jipya limekuja na sera ya kuwazuia 
watoto wao kwenda shule, hospitali kupata matibabu na kulipa nauli 
wanapokuwa katika vyombo vya usafiri, hatua inayopingana na azma ya 
Serikali kutaka watoto wapate haki zao za msingi. “Serikali haitakuwa 
tayari kuona baadhi ya watu wanazuia haki za msingi za watoto wao kwa 
kuwakataza kwenda shule, kupata matibabu katika hospitali au zahanati 
kwa kisingizio cha imani za kidini, jambo hili haliwezi kukubalika,” 
alisema Toyima.
Waumini hao wanaoshikiliwa na polisi katika Kituo 
Kikuu cha Polisi Kakonko wametajwa kuwa ni; Ndayizeye Gervas, Majaliwa 
Gervas, Paschal Silvanus, Inocent Ernest, Medadi Laurent na Julietha 
Medadi ambao ni wakazi wa Kijiji cha Nyabibuye, Kata ya Rumashi wilayani
 Kakonko na wote wanatarajiwa kufikishwa mahakamani kujibu tuhuma 
zinazowakabili.
Mkuu huyo wa wilaya, aliwataka wananchi kuachana 
na dini zisizoeleweka na zinazoleta mifarakano katika jamii, na wakati 
wengine wakisisitiza kuwapatia elimu watoto wao, kanisa hilo linakataza 
kusomesha watoto kwa madai kwamba kuwapeleka shule na hospitali ni 
dhambi kwa Mungu.
Alisema jitihada za Serikali wilayani Kakonko 
zimesaidia kuwachukua watoto wawili waliofaulu kwenda Sekondari za 
Kanyonza na Nyamtukuza na kuwawezesha kuanza masomo ya kidato cha 
kwanza.
Kanisa hilo jipya linadaiwa kujimega kutoka katika
 Kanisa la Sabato ambalo ni mojawapo ya makanisa yenye idadi ndogo ya 
waumini mkoani Kigoma ikilinganishwa na Kanisa Katoliki, Anglikana na 
Assemblies of God.
Chanzo;Mwananchi
Chanzo;Mwananchi
0 comments:
Post a Comment