Home » » Mfumo huu wa kuchuma, kula haumsaidii Mtanzania

Mfumo huu wa kuchuma, kula haumsaidii Mtanzania

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Watu wengi wanasema mzazi mwenye busara siku zote hujitahidi kuweka akiba kwa matumizi ya familia yake.
Akiba hiyo ndiyo huwa mkombozi kwa familia ile hasa wakati wa shida au hali ya hewa inapobadilika na mavuno kuwa haba.
Hata hivyo, kwa mtu ambaye ni mtumishi iwe serikalini au kokote kwingine katika Tanzania ni vigumu kwake kuweka akiba hasa kwa fedha inayopatikana kwenye mshahara na marupurupu mengine.
Swali la msingi ni kuwa je, anawezaje mtumishi wa serikali kuishi vizuri nchini Tanzania wakati ana kipato ambacho hakilingani au hakiendani na hali halisi ya maisha?
Pengine jiulize, anaishi vipi Mtanzania ambaye anachuma kiasi cha Sh200,000 kwa mwezi huku akiishi katika chumba cha kupanga, akinunua chakula na mahitaji mengine, akihitaji kusafiri kwenda na kurudi kibaruani kwake?
Kwa ufupi, hiki ni kitendawili ambacho kinawakabili watu wengi katika nchi hii, wakiwamo wakulima na wafanyakazi. Huenda kitendawili hiki kimewaepa wachache wakiwamo wafanyabiashara hasa wakubwa ambao hata hivyo ni wachache.
Wakati huu ambao kama si Bunge la Katiba ambalo linaendelea mjini Dodoma, watu wengi wangekuwa wameweka macho na masikio yao kwenye bajeti ya serikali ambayo kwa kawaida imekuwa ikisomwa mwezi Aprili.
Tofauti na miaka michache iliyopita ambako matumaini ya wengi yalikuwa ni kwenye hotuba ya bajeti ya Waziri wa Fedha, siku hizi wengi wanaisubiri hotuba hiyo ili kuhesabu ni kiasi gani cha maumivu wameongezewa katika maisha yao kwa njia mbalimbali, zikiwamo kodi za aina mbalimbali ambazo zimekuwa zikitangazwa kila mwaka.
Ukiwauliza watu wengi mijini na vijijini watakuambia kuwa afadhali ya jana kuliko leo. Kwa nini? Ni kwa kuwa hali ya maisha inazidi kudorora huku hali ya uchumi kwa mtu mmoja mmoja hadi kitaifa ikizidi kudhoofika.
Hivyo, kama Taifa, nadhani kuna mambo yamekwenda vibaya kiasi kwamba badala ya matumaini ambayo Watanzania wamekuwa wakipewa na wanasiasa hasa wakati wa uchaguzi, hali inakuwa kinyume chake.
Tatizo ni nini ? Je, kinachoiangusha nchi yetu ni sera na mipango mingi ambayo inaandaliwa na wataalamu wetu wakiwamo wachumi ambayo utekelezaji wake unategemea zaidi siasa?
Inawezekana kuwa ni kweli kwamba sera na mipango mingi inayopangwa kutoka juu kwenda chini badala ya mfumo shirikishi wa kuanzia kwenye familia moja, kwenda Serikali za Mitaa na kuendelea kuwa juu haufanyiki na badala yake wananchi wote bila kujali tofauti zao za kimazingira, jiografia, uchumi wanalazimika kutekeleza sera zinazoandaliwa mijini.
Tatizo la mifumo hii ni kwamba wananchi wanalazimika kutekeleza mipango mingi ambayo haiwahusishi kwa kiasi kikubwa na matokeo yake inapokwama hawana mahali pa kukimbilia.
Ni dhahiri kwamba kwa zaidi ya miaka 50 ya uhuru wa nchi hii, wananchi wameendelea kuambiwa maneno na kaulimbiu zinazofanana kwamba kilimo ndiyo uti wa mgongo wa Watanzania.
Lakini, je, kilimo hiki cha jembe la mkono ambacho si cha kuwezesha kulima na kupata ziada kinaweza kumsaidia vipi mwananchi wa Tanzania kujikwamua kimaisha?
Nimesoma mahali kauli ya maaskofu wa Kanisa Katoliki Tanzania kupitia baraza lao, TEC ambao wanaeleza kuwa kilimo siku hizi ni cha kubabaisha, kibaguzi hasa kwa kuzingatia ukweli kuwa wakulima wameporwa ardhi kwa kisingizio cha uwekezaji, hili ni jambo ambalo linaumiza.
Chanzo;mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kigoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa