Home » » Wenye kisukari hatarini kwa maradhi ya kinywa

Wenye kisukari hatarini kwa maradhi ya kinywa

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Watu wanaougua ugonjwa wa kisukari wako katika hatari zaidi kupata magonjwa ya kinywa na meno, kwa sababu sukari ina nafasi kubwa katika kusababisha magonjwa hayo.
Hayo ni kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa na Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na kueleza kuwa asilimia 60 ya Watanzania wana matatizo ya kinywa na meno.
Akizungumzia uhusiano kati ya kisukari na magonjwa ya meno, Mtaalamu kutoka Idara ya Sukari Hospitali ya Muhimbili, Dk Zulfiqarali Abbas alisema ugonjwa wa kisukari huathiri kinga ya mwili, ambapo baadaye viungo vya mwili huathirika pia.
“Sukari ni adui mkubwa pia wa meno, lazima watu wapunguze kula sukari na kusafisha meno yao. Hii itawafanya kuwa salama licha ya kuugua kisukari,” alisema Dk Abbas.
Abbas aliwatoa hofu wagonjwa wa kisukari kuwa dawa wanazozitumia hazisababishi magonjwa ya kinywa na meno, hivyo wazingatie kumaliza dawa ili kutibu maradhi yao.
Nao madaktari kutoka Hospitali ya IMTU wamezungumzia mambo mbalimbali yanayosababisha matatizo hayo, ikiwamo ulaji mbaya wa vyakula vya sukari na uvutaji wa sigara na unywaji wa pombe.
Dk. Ally Mzighe alisema watu wamekuwa hawasafishi vinywa vyao ipasavyo ili kuviweka katika hali ya usafi na kuepuka bakteria hatari wanaosababisha meno kutoboka, kuvimba fizi na baadaye kupata kansa.
Mzighe aliwataka wazazi pia kuwa makini katika kusimamia usafi wa vinywa vya watoto wao, ambao wameanza kuota meno ili kuwaepusha na bakteria hatari ao.
Naye Dk. Gregory Mandari alisisitiza umuhimu wa kufanya uchunguzi wa meno mara kwa mara, ili kujua tatizo na kulipatia ufumbuzi wa haraka .
Dk. Mandari ambaye ni mtaalamu wa magonjwa ya kinywa na meno katika Hospitali ya IMTU alisema Watanzania wengi hawana mwamko wa kufanya usafi wa kinywa, matokeo yake huenda hospitali wakati tatizo limekuwa kubwa.
“Kwa mwezi huwa ninapata watu wawili tu wanaokuja kufanyiwa uchunguzi meno yao, wengine wengi huja hospitali kung’oa meno yaliyokwisha toboka na kuathirika sana,” alieleza Dk Mandari.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kigoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa