Home » » JPM KUANZA ZIARA SIKU TATU KIGOMA

JPM KUANZA ZIARA SIKU TATU KIGOMA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

 Imeandikwa na Fadhili Abdallah, Kigoma
Rais wa Tanzania, Dk John Pombe Magufuli.
RAIS John Magufuli anatarajia kuanza ziara ya siku tatu mkoani Kigoma kuanzia kesho ambayo akiwa mkoani humo, kiongozi huyo wa nchi anatarajia kuweka mawe ya msingi kwenye miradi ya ujenzi wa barabara na miradi ya maji.
Akitoa taarifa kwa waandishi wa habari jana, Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Emmanuel Maganga alisema Rais Magufuli atawasili kesho akitokea Kagera, na katika siku yake ya kwanza anatarajiwa kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa barabara ya kiwango cha lami kutoka Nyakanazi, Biharamulo mkoani Kagera hadi Kakonko mkoani hapa.
Maganga alisema baada ya kuweka jiwe la msingi la mradi huo, Rais Magufuli atahutubia mkutano wa hadhara Kakonko Mjini akiwa njiani kwenda wilayani Kasulu ambako ataweka jiwe la msingi la ujenzi wa barabara ya kiwango cha lami kutoka Kidahwe hadi Uvinza.
Aidha, siku ya pili ya ziara hiyo, Rais Magufuli atatembelea kukagua maendeleo ya mradi mkubwa wa maji unaotekelezwa kwa ufadhili wa Serikali ya Ujerumani katika Manispaa ya Kigoma Ujiji akihitimisha ziara yake ya siku hiyo kwa kuwa na mkutano wa hadhara kwenye Uwanja wa Lake Tanganyika mjini Kigoma.
Mkuu huyo wa mkoa alisema katika siku yake ya mwisho mkoani Kigoma, Dk Magufuli ataweka jiwe la msingi la mradi wa maji katika Mji Mdogo wa Nguruka na kuhutubia mkutano wa hadhara, na baada ya mkutano huo atakwenda mkoani Tabora kuendelea na ziara yake.
CHANZO HABARI LEO.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kigoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa