Na Mwandishi Wetu, Kigoma Yetu
JESHI la polisi Mkoa wa Kigoma kwa kushirikiana na hifadhi ya Taifa Tanapa mkoani hapa wamefanikiwa kumkamata mtuhumiwa mmoja akiwa na risasi 380 na bunduki aina ya SMG namba UG1241-1998 yenye magazine mbili Mkoani Geita.
Taarifa hiyo imetolewa na Mratibu Mwandamizi wa Jeshi la Polisi SSP Dismasi Kisusi jana kwa vyombo vya habari mkoa wa Kigoma na kusema kuwa mtuhumiwa huyo alikamatwa katika mkoa wa Geita maeneo ya Runzewe akiwa na mzani wa kupimia meno ya tembo pamoja na risasi hizo.
SSP Kisusi alimtaja mtuhumiwa huyo kuwa ni Samson Emmanuel (33) mkazi wa Mvugwe Wilaya ya Kasulu mkoa Kigoma ambaye anajihusisha na uuzaji na usafirishaji wa silaha za kivita kutoka nchi jirani na kuziingiza nchini Tnzania.
Aidha alisema kuwa mtuhumiwa huyo pia aliwahi kufunguliwa jalada namba KBO/IR/1022/2011na kupelekwa katika mahakama ya Wilaya ya Kibondo mkoani Kigoma na kufunguliwa kesi namba CC 248/2011 kwa kosa la kumiliki silaha aina ya SMG 0382 kinyume cha sheria ambapo alitokomea kusiko julikana na kesi hiyo kutosikilizwa.
Hta hivyo mtuhumiwa huyo aliyekuwa akisafirisha risasi 990 za silaha za kivita aina ya SMG/ SAR aliwatoroka askari polisi wakiwa doria na kutelekeza baiskeli iliyokuwa imebeba risasi hizo katika kijiji cha Mvugwe Tarafa ya Makere Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma.
Kwa upande wake Muhifadhi Mkuu hifadhi ya Taifa ya Gombe bi. Noeliya Muyonga aliwataka wananchi kutoa ushirikiano katika kukabiiliana na wahalifu wanaoleta madhara kwa wanyama poli pamoja na watalii wa hifadhi hizo.
Bi. Muyonga alisema kuwa kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo ni kutokana na ushirikiano baina ya Jeshi la polisi, kikosi dhidi ya ujangili kanda ya Tabora na kikosi cha kupambana na ujangili FCF Wilaya ya Kasulu ambapo mtuhumiwa huyo amekuwa akifanya matukio mbalimbali katika hifadhi hizo.
Blogzamikoa
0 comments:
Post a Comment