Home » » Washauriwa kufuga samaki

Washauriwa kufuga samaki

Kigoma. Wakazi wa Mkoa wa Kigoma, wametakiwa kujikita katika ufugaji wa samaki kwa kuzingatia kuwa mkoa huo una maji na ardhi ya kutosha kufanya shughuli hizo.
Wito huo ulitolewa juzi na Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila, alipokuwa akizungumza na Mwananchi kuhusu mikakati ya kuondoa umaskini katika jamii.
Alisema ingawa Mkoa wa Kigoma una  mabwawa katika sehemu mbalimbali, lakini ufugaji wa samaki bado ni wa kiwango cha chini.
“Haiwezekani wananchi waliopo kwenye fursa kama hii ya kwetu (Kigoma) washindwe kufuga samaki kikamilifu na badala yake wanategemea zaidi samaki kutoka Ziwa Tanganyika ambako uvuvi unaofanyika ni wa kizamani sana,” alisema Kafulila.
 Aliwataka maofisa kilimo na mifugo kuwa chachu kwa kuwaelimisha wananchi juu ya ufugaji wa samaki  utakaosaidia kuinua vipato vyao.
Kafulila pia alishauri halmashauri za wilaya na manispaa mkoani Kigoma, kufikiria namna ya kuwajengea uwezo watu ili hatimaye, wamudu kuanzisha miradi ya kufuga samaki.
Kuhusu  ufugaji wa ng’ombe mkoani humo, alisema bado ni wa kiwango cha chini. “Ufugaji wa ng’ombe ni rasilimali muhimu katika jamii na maeneo ambayo Serikali Kuu na halmashauri zimeweka utaratibu mzuri zimejikuta zikipata mafanikio makubwa ya kiuchumi na kijamii,” alisema Kafulila.
 Aliisihi Serikali kuweka mifumo thabiti ya kuwakomboa wafugaji ili waweze kufuga kitaalamu na kwa kiwango bora kinachokubalika na hatimaye kuwawezesha kupata fedha.   
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kigoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa