Home » » Machali wa NCCR azomewa

Machali wa NCCR azomewa

MBUNGE wa Kasulu Mjini mkoani Kigoma, Bw. Moses Machali (NCCR-Mageuzi), juzi amejikuta akizomewa baada ya kutoa kauli za kuwaponda baadhi ya viongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).

 Bw. Machali alipatwa na kadhia hiyo katika stendi ya zamani iliyopo Mjini Nansio, Wilaya ya Ukerewe, mkoani Mwanza wakati akihutubia mkutano wa hadhara.
Akiwa jukwaani, Bw. Machali alijikuta akizomewa kila alipotoa kauli za kuelezea maovu ya viongozi wa CHADEMA hasa alipozielekeza kwa Mwenyekiti wake, Freeman Mbowe.
Katika mkutano huo, mbunge huyo alisema hakuna watu wabaya kama viongozi wa CHADEMA hasa Bw. Mbowe ambaye pia ni Kiongozi wa Kambi ya Upinzani bungeni.
Alisema Bw. Mbowe aliwahi kusimama bungeni na kutaka matumizi mabaya ya fedha za Serikali na ununuzi wa magari ya kifahari yakome lakini baada ya kurudisha gari alilopewa na Serikali alilifuata na kuendelea kulitumia.
Kauli hiyo na nyingine za kuwatuhumu baadhi ya wabunge wa CHADEMA kushiriki katika ufisadi hasa wa kupokea posho za kwenda nje ya nchi, zilisababisha Bw. Machali azomewe baadhi ya watu wakimtaka afunge mkutano na kuondoka.
Kelele za kushinikiza aondoke zilimfanya akatishe hotuba yake mara kwa mara baadhi ya watu wakidai alitumwa na wabaya wa CHADEMA ili kuwaponda viongozi wao.
Kutokana na shinikizo hilo, Bw. Machali alisema ataendelea kuzungumza ukweli kuhusu kiongozi na mtu yeyote mwenye mienendo isiyofaa bila kujali ni kiongozi kutoka chama gani.
Hata hivyo, utulivu ilirejea aliposema 'People' na wananchi kumjibu 'Power', ndipo akaendelea na mkutano wake akiituhumu Serikali kwa kushindwa kuboresha maisha ya Watanzania badala yake inawabebesha mzigo mkubwa wa kodi.
Alionya kuwa, Taifa haliwezi kupata maendeleo kama Serikali itaendelea kuingia mikataba mibovu ya uchimbaji madini na kuwanufaisha watu wachache.

Chanzo;Majira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kigoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa