Home » » WIKI YA TAFAKURI KATIKA SECTA YA ELIMU

WIKI YA TAFAKURI KATIKA SECTA YA ELIMU

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Inaadhimishwa  nchini kote kuanzia ngazi ya wilaya hadi Taifa. Ni wiki inayowakutanisha pamoja wadau kujadili maendeleo ya Sekta ya Elimu
Ni tukio la kwanza la aina yake nchini litakaloshuhudia wadau muhimu wa elimu wakipongezwa kwa mafanikio yao katika kuiendeleza Sekta ya Elimu.
 Katika wiki hii, iliyoanza Mei 3 na   ambayo itahitimishwa kitaifa Mei 10, harakati zake zinaelezwa kuanzia katika ngazi za halmashauri, mkoa na hatimaye taifa.
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Dk Shukuru  Kawambwa  anasema, pamoja na mambo mengine, Wiki ya Elimu inalenga kuunganisha nguvu na mawazo ya wadau kuelekea upatikanaji wa elimu bora.
“Lengo la kuwa na Wiki ya Elimu ambayo itakuwa ikiadhimishwa kila mwaka, ni kuelimisha umma juu ya umuhimu wa elimu bora na kuhamasishana kuchochea ari ya ushindani wa kitaaluma kwa wadau mbalimbali wa elimu,   wakiwamo walimu, wanafunzi, wazazi na jamii kwa jumla,” anasema .
“Kaulimbiu ya mwaka huu ni ‘Elimu Bora kwa Wote Inawezekana, Timiza Wajibu Wako’.”
Wasaa wa tafakuri
Meneja mawasiliano na utetezi katika Ofisi ya Rais, Usimamiaji wa Utekelezaji wa Miradi (PDB), Hassan Abbas anasema Wiki ya Elimu ni wasaa mzuri kwa wananchi kufanya tafakuri ya safari ya kuboresha elimu yao.
“Ni kipindi cha tafakuri kwa sababu sote tunafahamu kuwa elimu bora ndio ukombozi wa Taifa hili katika kutoa wataalamu wa nyanja na fani mbalimbali,’’ anaeleza.
Ni dhahiri kuwa kila mtu angependa kuona nchi inapiga hatua kubwa ya mafanikio katika njanja zote. Mafanikio hayo yatatokana na mfumo mzuri wa elimu unaotoa wahitimu wenye stadi muhimu na sahihi.
Abbas anaongeza: “Wiki ya Elimu inatupa fursa maridhawa kwa sote kujiuliza tunafanya nini katika kufikia elimu bora, ambayo Mwalimu Julius Nyerere aliwahi  kuifafanua kuwa ni ile inayompa mtu stadi muhimu za kuyamudu maisha yake.
“Ni dhahiri kuwa kila mmoja wetu ana kitu cha kuchangia. Hivyo lengo la wiki hii litatimia iwapo kila mhusika atachangia mawazo yake katika kuboresha sekta ya elimu. ‘’
Tuzo na motisha
Sambamba na mijadala kuhusu mustakabali wa elimu, Wiki ya Elimu itatumika kutoa tuzo kwa halmashauri, shule na wanafunzi waliofanya vizuri katika mitihani ya taifa mwaka jana.
Ofisa elimu mkuu katika Kitengo cha Usimamizi wa Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa, Hilda Mkandawile anasema tuzo itakuwa za fedha na zisizo za fedha.
Anasema tuzo hizo zitatolewa katika makundi matano ambayo ni shule zilizofanya vizuri katika mtihani wa mwaka 2013 na zilizoonyesha  maendeleo ya juu kwa kulinganisha matokeo ya mwaka 2012 na 2013.
Makundi mengine ni wanafunzi waliofanya vizuri katika mitihani ya kumaliza elimu ya msingi na sekondari mwaka 2013, na Mkoa na Halmashauri iliyofanya vizuri katika taaluma. 
Pia kutakuwa na tuzo kwa wanafunzi walioshinda katika mashindano ya insha za jumuiya ya SADC  na Open Goverment Partnership  (OGP).
Mafanikio ya Mpango wa GRN
Kupitia utekelezaji wa Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (GRN) ulioanza mwezi Aprili mwaka jana, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi na vyombo inavyovisimamia inajivunia mafanikio kadhaa ya kutia moyo katika sekta ya elimu.
Kwa mfano, mkakati wa kuzipanga shule kitaifa kwa kuzingatia ubora wa ufaulu wa shule katika mtihani, umeleta hamasa kubwa na kukuza ari ya wadau wa shule kuhakikisha shule zao zinafanya vizuri hivyo kupanda daraja la ufaulu kitaifa, kwa mujibub wa kaimu katibu mtendaji wa Baraza la Mitihani Tanzania (Necta), Dk Charles Msonde.
 “Baraza la Mitihani limeandaa vitabu vya mwongozo wa upangaji wa shule katika makundi ya ufaulu kwa madhumuni ya kuwawezesha wadau wote wa elimu kufahamu  jinsi upangaji wa shule kwa ubora wa ufaulu unavyofanywa,’’ anafafanua.
Mafanikio mengine anayotaja Dk Msonde ni kufanya upembuzi wa kubaini makosa yanayofanywa na watahiniwa na kutoa mwongozo kwa wadau kama sehemu ya kukabiliana na tatizo la watahiniwa kutojibu maswali ipasavyo.
“ Baraza limeandaa na kusambaza kwa wadau wa elimu vitabu vya uchambuzi wa ufaulu wa watahiniwa kwa kila swali kwa shule za msingi na sekondari kwa masomo yote, ili walimu na wanafunzi waweze kufahamu changamoto zilizopo wakati wa kujibu  maswali ya mitihani, hivyo kujifunza mbinu bora za kujibu maswali,’’ anaeleza.
Wizara pia imejifunga kibwebwe ikishupalia kupunguza na kumaliza tatizo la wanafunzi wa shule za msingi, wakiwamo wahitimu wa darasa la saba kushindwa kujua kusoma, kuandika na kuhesabu.
Ili kukabiliana na hali hiyo, Wizara inatekeleza mkakati wa  Upimaji wa Stadi za Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK) wenye lengo la kuwapima wanafunzi  kwa ngazi ya shule na kitaifa kuhusu kumudu  stadi hizo.
Kaimu mkurugenzi wa Elimu ya Msingi, Sara Mlaki anasema upimaji wa kitaifa wa stadi za  KKK ulifanyika Julai mwaka 2013 kwa kutumia zana za kimataifa kwa lengo la kufuatilia viwango vilivyofikiwa na wanafunzi katika shule za msingi kuhusu stadi za kusoma, kuandika na ufanyaji wa hesabu.  Jumla ya wanafunzi 2,266 kutoka shule 200 na Halmashauri 20 walishiriki katika upimaji huo.
Akizungumzia matokeo,  Mlaki anasema asilimia 40 ya wanafunzi hawakuweza kujibu angalau swali moja kwa ufasaha na asilimia 8  ya wanafunzi wa darasa la pili walikuwa wakisoma na kuelewa.
Kuhusu tathmini ya kusoma Kiingereza, ilionyesha kuwa watoto wanajifunza Kiingereza kwa mara ya kwanza wakiwa darasa la pili na wanajifunza kama somo, hivyo siyo jambo la kushangaza kwamba baada ya mwaka mmoja bado watoto wengi wanakosa ufahamu wa lugha hiyo.
“Tathmini ya Hisabati ilibainisha kwamba wanafunzi wanafanya vizuri zaidi katika maarifa ya akili (wanakumbuka) vitu, lakini hawafanyi vizuri katika maswali ya kuelewa zaidi na kutumia maarifa yao ya kiakili, huku mkazo wa ufundishaji wa somo hilo ukizama zaidi katika kukariri vipengele na kanuni,’’ anaeleza Mlaki.
Matokeo ya tathmini hii bila shaka yanashadadia ukweli kuwa KKK bado ni changamoto tete katika mfumo wa elimu. Hili ni moja ya matatizo lukuki yanayopaswa kufanyiwa tafakuri ya kina na wadau wa elimu hasa katika wiki hii ya elimu.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kigoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa